[1] [2] [3] [4] [5]

Chapter 5

1: Ndugu, hakuna haja ya kuwaandikieni juu ya nyakati na majira yatakapotukia mambo haya. 2: Maana ninyi wenyewe mwajua kwamba Siku ya Bwana itakuja kama mwizi ajavyo usiku. 3: Watu watakapokuwa wanasema: "Kila kitu ni shwari na salama" ndipo uharibifu utakapowaangukia ghafla! Mambo hayo yatatukia ghafla kama uchungu wa uzazi unavyomjia mama anayejifungua, wala watu hawataweza kuepukana nayo. 4: Lakini ninyi ndugu, hamko gizani, na siku hiyo haipaswi kuwajieni ghafla kama vile mwizi. 5: Ninyi nyote ni watu mnaoishi katika mwanga, watu wa mchana. Sisi si watu wa usiku, wala wa giza. 6: Basi, tusilale usingizi kama wengine; tunapaswa kukesha na kuwa na kiasi. 7: Wanaolala hulala usiku, na walevi hulewa usiku. 8: Lakini sisi ni watu wa mchana na tunapaswa kuwa na kiasi. Tunapaswa kuvaa imani na upendo kama vazi la kujikinga kifuani, na tumaini letu la wokovu kama kofia ya chuma. 9: Maana Mungu hakututeua ili tuangamizwe na ghadhabu yake, bali tuupate wokovu kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, 10: ambaye alikufa kwa ajili yetu, ili tuishi pamoja naye, iwe tu hai au tumekufa. 11: Kwa hiyo farijianeni na kusaidiana ninyi kwa ninyi kama mnavyofanya sasa. 12: Ndugu, tunawaombeni muwastahi wale wanaofanya kazi kati yenu, wale wanaowaongoza na kuwafundisheni kuhusu maisha ya Kikristo. 13: Wapeni heshima kubwa na kuwapenda kwa sababu ya kazi wanayofanya. Muwe na amani kati yenu. 14: Ndugu, tunawahimizeni muwaonye watu walio wavivu, muwatie moyo watu wanyonge, muwasaidie watu dhaifu, muwe na subira kwa wote. 15: Angalieni mtu yeyote asimlipe mwingine maovu kwa maovu, ila nia yenu iwe kutendeana mema daima na kuwatendea mema watu wote. 16: Furahini daima, 17: salini kila wakati 18: na muwe na shukrani katika kila hali. Hayo ndiyo anayotaka Mungu kwenu katika kuungana kwenu na Kristo Yesu. 19: Msimpinge Roho Mtakatifu; 20: msidharau unabii. 21: Pimeni kila kitu: zingatieni kilicho chema, 22: na epukeni kila aina ya uovu. 23: Mungu anayetupatia amani awafanye ninyi watakatifu kwa kila namna na kuzilinda nafsi zenu--roho, mioyo na miili yenu--mbali na hatia yoyote wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo. 24: Yeye anayewaita ninyi atafanya hivyo kwani ni mwaminifu. 25: Ndugu, tuombeeni na sisi pia. 26: Wasalimuni ndugu wote kwa ishara ya upendo. 27: Nawahimizeni kwa jina la Bwana muwasomee ndugu zetu wote barua hii. 28: Tunawatakieni neema ya Bwana wetu Yesu Kristo.